Shirika la ndege la taifa la Tanzania, Air Tanzania, limetangaza mpango maalum wa kuwarejesha nyumbani raia wa Tanzania waliokwama katika eneo la Mashariki ya Kati kufuatia kusitishwa kwa safari nyingi za ndege kutokana na mgogoro unaoendelea kati ya Israel, Iran na Marekani.
Katika taarifa iliyotolewa leo Ijumaa, Machi 6, shirika hilo limesema litaendesha safari maalum ya ndege kutoka Dar es Salaam kwenda Dubai kwa lengo la kuwachukua Watanzania waliokwama katika eneo hilo na kuwarejesha nchini. Ndege hiyo inatarajiwa kuondoka Dar es Salaam na kisha kurejea tena nchini siku ya Jumapili baada ya kukamilisha zoezi la kuwachukua abiria.
Air Tanzania imesisitiza kuwa safari hiyo haitakuwa ya kibiashara, bali ni operesheni maalum ya dharura kwa ajili ya kusaidia wananchi waliokumbwa na athari za kusimamishwa kwa safari nyingi za kimataifa katika eneo la Ghuba. Shirika hilo limeongeza kuwa kipaumbele kitapeanwa kwa wasafiri ambao tayari walikuwa wamekata tiketi kabla ya safari kusitishwa kutokana na hali ya usalama kuzorota.
Hatua hiyo imekuja wakati mashirika mengi ya ndege duniani yakiahirisha au kusitisha safari zake kuelekea Mashariki ya Kati kufuatia kuongezeka kwa mvutano wa kijeshi. Mvutano huo ulianza baada ya Marekani na Israel kuanzisha mashambulizi dhidi ya Iran mapema Jumamosi iliyopita, jambo lililosababisha Iran kujibu kwa mashambulizi katika maeneo mbalimbali ya kanda ya Ghuba.
Chanzo; Global Publishers