Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetahadharisha kuwepo na uwezekano wa mvua kubwa, upepo mkali na mawimbi makubwa baharini.
Taarifa iliyotolewa na TMA leo Ijumaa Oktoba 24, 2025, imesema mvua hizo zitakazoambatana na upepo mkali unasababishwa na kimbunga kinachojulikana kama Tropical Storm Chenge ambacho kinatarajiwa kuathiri maeneo kadhaa nchini, ikiwemo Mkoa wa Dar es Salaam.
Mikoa mingine iliyotajwa ni Mtwara, Lindi, Pwani na Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba inatarajiwa kupata mvua kubwa kuanzia Oktoba 26 hadi 28, mwaka huu.
TMA imesema utabiri wa hali ya hewa unaonyesha kuwa kimbunga hicho kinaendelea kusogea upande wa magharibi mwa Bahari ya Hindi huku kikipungua nguvu taratibu kadri kinavyokaribia pwani ya Tanzania.
“Hali hii inatarajiwa kusababisha ongezeko la mvua, upepo mkali na mawimbi makubwa katika maeneo ya ukanda wa pwani,” imesema sehemu ya taarifa ya TMA.
Chanzo: Mwananchi