Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limepokea magari mapya aina ya Robur Armored TLC300 kama mgao kutoka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini.
Akizungumza mara baada ya kupokea magari hayo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Benjamin Kuzaga amemshukuru Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa vitendea kazi vitakavyotumika kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao Mkoa wa Mbeya.
Kamanda Kuzaga amesisitiza kuwa magari hayo yatatumika kikamilifu katika kubaini, kuzuia na kutanzua uhalifu ndani ya Mkoa wa Mbeya na kuahidi kuyatunza ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa na Jeshi la Polisi na Serikali.
Chanzo: Clouds Media