Mkazi wa Mtaa wa Ulkung’ uliopo Kata ya Terat, jijini Arusha, Cleofasi Oiso (35) amefariki dunia baada ya kudaiwa kujinyonga nyumbani kwake, huku chanzo kikitajwa kuwa mgogoro wa kifamilia uliotokana na kushindwa kulipa mahari ya mkewe, ambaye wameishi naye kwa miaka minane.
Taarifa zinaeleza kuwa Oiso, aliyekuwa fundi wa kuchomelea alikuwa akiishi na mkewe Anderika Kessy (32) na watoto wao wawili.
Inadaiwa kuwa mgogoro kati yao ulizidi baada ya mkewe kumtaka alipe mahari hata kwa awamu, jambo lililodaiwa kumletea shinikizo kubwa kutokana na hali yake ya kiuchumi.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo amesema tukio hilo limetokea jana Desemba 26, 2025 na kwamba, mwili wa marehemu umekutwa ndani ya nyumba yao. Amesema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo halisi cha tukio hilo.
Kwa mujibu wa taarifa za jirani na viongozi wa mtaa, kabla ya tukio hilo Oiso alilalamikia mgogoro wake kwa jirani yake na baadaye akamshirikisha Balozi wa mtaa huo, ambaye aliahidi kuitisha kikao cha usuluhishi saa 12 jioni siku hiyo. Hata hivyo, Oiso alifariki kabla ya muda wa kikao hicho kufika.
Akizungumza nyumbani hapo leo Jumamosi Desemba 27, 2025, mke wa marehemu, akiyejitambulisha kwa jina la Anderika, amesema wameishi pamoja kwa miaka minane bila kulipiwa mahari.
Chanzo; Mwananchi