Tanzania imeungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha Siku ya Wanyamapori Duniani, siku maalum inayotambua mchango wa wanyamapori katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kimazingira.
Akizungumzia maadhimisho hayo mkoani Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii nchini (TTB), Ephraim Mafuru, amesema kwa Tanzania wanyamapori si urithi wa asili pekee, bali ni sehemu muhimu ya utambulisho wa taifa.
“Wanyamapori ni uti wa mgongo wa sekta yetu ya utalii. Ni chanzo cha ajira na kipato kwa maelfu ya wananchi, na ni fahari inayolitangaza taifa letu kimataifa,” amesema Mafuru.
Ameeleza kuwa kupitia rasilimali hizo za asili, nchi imeendelea kuwa miongoni mwa vivutio vinavyoongoza duniani kwa utalii wa wanyamapori, ikivutia wageni kutoka pande mbalimbali za dunia kuja kujionea na kufurahia vivutio vya kipekee vilivyopo nchini.
Mafuru amesisitiza kuwa TTB itaendelea kuhamasisha na kukuza utalii endelevu unaolinda mazingira, kuheshimu bioanuwai, na kuhakikisha wanyamapori wanahifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Chanzo; Nipashe