Search

Saved articles

You have not yet added any article to your bookmarks!

Browse articles

GDPR Compliance

We use cookies to ensure you get the best experience on our website. By continuing to use our site, you accept our use of cookies, Privacy Policy, and Terms of Service.

Iran Yakanusha Kuishambulia Oman, Yaibebesha Israel Mzigo

Makao Makuu ya Jeshi la Wanajeshi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yamepinga vikali madai ya kuhusika na mashambulizi ya kijeshi dhidi ya ardhi au bandari za Usultani wa Oman, kufuatia taarifa za mashambulizi ya ndege zisizo na rubani katika bandari za Duqm na Salalah.


Kupitia taarifa iliyotolewa na Kituo chake cha Mawasiliano, jeshi hilo limesema halijahusika kwa namna yoyote na kile kilichoelezwa kama uchokozi dhidi ya “rafiki na jirani” yake, Oman. Kauli hiyo imekuja wakati miundombinu ya nishati katika ukanda huo ikiripotiwa kushambuliwa na ndege za angani katika matukio ambayo bado hayajaelezewa kikamilifu.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Oman, tanki la mafuta katika bandari ya kibiashara ya Duqm lililengwa na ndege kadhaa zisizo na rubani siku ya Jumanne. Mamlaka zilisema moto uliosababishwa na shambulio hilo ulidhibitiwa bila kusababisha vifo, ingawa tukio hilo ni la pili ndani ya wiki hii. Siku ya Jumapili, ndege mbili zisizo na rubani zilishambulia eneo hilo na kumjeruhi mfanyakazi mmoja.


Serikali ya Oman pia iliripoti kuwa ndege mbili nyingine zisizo na rubani zilidunguliwa juu ya Mkoa wa Dhofar siku ya Jumanne, huku ndege ya tatu ikianguka karibu na bandari ya Salalah.

Makao Makuu ya Khatam al-Anbiya, kamandi kuu ya pamoja ya majeshi ya Iran, yalitoa tamko yakidai kuwa mashambulizi dhidi ya mataifa ya Kiislamu ni “jaribio la kukata tamaa” la Marekani na Israel kwa lengo la kuharibu sifa ya Iran kimataifa.
“Wazayuni wavamizi na Wamarekani wanakusudia kushambulia vituo vya kidiplomasia na maslahi ya nchi za Kiislamu katika eneo hili ili kuilaumu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran,” tamko hilo lilisema.

Aidha, jeshi hilo lilisisitiza kuwa operesheni zake zinaendeshwa kwa umakini na nidhamu ya hali ya juu, likieleza kuwa mashambulizi yake yanalenga tu “utawala wa Kizayuni pamoja na majeshi ya Marekani na miundombinu yao ya kijeshi, kiusalama na maslahi yao.”
Kwa mujibu wa Khatam al-Anbiya, mashambulizi dhidi ya nchi jirani zisizoegemea upande wowote ni mkakati wa kuisaidia Marekani na Israel kujinasua katika mkwamo wa sasa.

Wakati huo huo, Qatar ilitangaza kusimamisha uzalishaji wa gesi asilia iliyoyeyushwa (LNG), ambayo inachangia takribani asilimia 20 ya usambazaji wa dunia, huku Saudi Arabia ikisema imesitisha shughuli katika kiwanda chake kikubwa zaidi cha kusafisha mafuta.


Katika Falme za Kiarabu (UAE), serikali ya Abu Dhabi ilithibitisha kuzuka kwa moto katika kituo cha matanki ya mafuta cha Musaffah kufuatia shambulio la ndege isiyo na rubani siku ya Jumatatu, ingawa ilisema shughuli hazikuathiriwa.

Iran imerudia msimamo wake kwamba haina uadui na nchi jirani za Kiislamu na inaendelea kujizatiti kulinda usalama wa ukanda huo, ikisisitiza kuwa mashambulizi yake ya kulipiza kisasi yanalenga tu mali na maslahi ya Marekani na Israel katika eneo hilo.

Kuhusiana na mada hii: