China imezitaka Iran, Marekani na Israel kusitisha mara moja mapigano yanayoendelea, ikionya kuwa mzozo huo unaweza kusababisha athari kubwa kwa uchumi wa dunia iwapo utaendelea kushika kasi.
Wito huo umetolewa leo Jumatano Machi 4, 2026 na msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Lin Jian, kupitia ujumbe aliouchapisha katika mtandao wa kijamii wa X, akisisitiza umuhimu wa kulinda usalama na utulivu wa eneo la Ghuba.
“China inazitaka pande husika kusitisha mara moja operesheni za kijeshi, kuepuka kuendeleza mvutano na kuzuia machafuko ya kikanda yasije yakasababisha madhara makubwa zaidi kwa ukuaji wa uchumi wa dunia,” ameandika Lin Jian.
Amesema Mlango wa Bahari wa Strait of Hormuz, ambao Iran ina ushawishi juu ya sehemu yake, ni njia muhimu ya kimataifa kwa usafirishaji wa bidhaa na nishati, hivyo kulinda usalama wake ni masilahi ya jumuiya ya kimataifa.
Kwa mujibu wa takwimu za biashara ya nishati, takribani nusu ya mafuta yote yanayoagizwa na China kutoka nje hupitia katika Mlango wa Hormuz. Aidha, asilimia 29 ya gesi asilia kimiminika (LNG) inayoagizwa na Taifa hilo hupitia njia hiyohiyo.
Zaidi ya asilimia 20 ya mafuta ya dunia hupitia katika Mlango wa Hormuz, hali inayoufanya kuwa kitovu muhimu cha biashara ya nishati kimataifa. Tangu kuanza kwa vita dhidi ya Iran mwishoni mwa wiki iliyopita, shughuli za usafirishaji katika njia hiyo zimeripotiwa kuvurugika kwa kiasi kikubwa.
Chanzo; Mwananchi