Kiongozi wa genge la dawa za kulevya la Jalisco New Generation, Nemesio Oseguera Cervantes, maarufu El Mencho, amezikwa jana Jumatatu katika jeneza la dhahabu linalong’aa, likiwa limezungukwa na mashada makubwa ya maua na ulinzi mkali.
Mazishi hayo yamevutia hisia mchanganyiko ya heshima, hofu na sintofahamu kwa wakazi wa jimbo la Jalisco.
Jeneza hilo lilielezwa kuwa la kifahari lenye mvuto wa macho, likiwa na umbo la kisasa na pembe zilizochongwa kwa ustadi.
Mng’ao wake uliakisi mwanga, likifanya mazishi yawe kielelezo cha utajiri na hadhi ya kipekee ya kiongozi aliyezikwa.
Gharama ya jeneza hili, lililopakwa dhahabu (gold-plated), inakadiriwa kufikia dola 20,000 za Marekani (takribani Sh50 milioni).
Ofisa mmoja wa Serikali alithibitisha kuwa mazishi yamefanyika katika makaburi ya Zapopan, kitongoji cha Guadalajara, jiji la pili kwa ukubwa nchini Mexico.
Chanzo; Mwananchi