Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Samia Suluhu Hassan, amewataka vijana wa Kitanzania kuendelea kuwa wazalendo, kulinda amani na kuipenda nchi yao, akisema Tanzania ni miongoni mwa mataifa bora na salama zaidi barani Afrika.
Akizungumza leo katika mkutano mkubwa wa kampeni uliofanyika Viwanja vya Tanesco, Temeke, jijini Dar es Salaam, Samia alisema Tanzania imebarikiwa kuwa nchi yenye utulivu, umoja na dira thabiti ya maendeleo, hivyo ni jukumu la vijana kuhakikisha wanaendelea kuiheshimu na kuithamini.
“Lakini vijana wa Kitanzania, msidanganywe. Ukichukua Afrika Mashariki, pengine hadi kusini na kati, Tanzania ni pepo. Hapa mpo kwenye nchi yenye jina, sifa na dira ya kuendeleza watu wake.
Msidanganywe, wale walioko nje wasiwadanganye. Hapa mko pazuri kweli kweli,” amesema Samia.
Ameongeza kuwa Tanzania ni mali ya wananchi wote, si ya mtu binafsi wala kundi fulani, akiwataka vijana kuilinda amani na umoja wa taifa. “Hii nchi ni yenu, si mali ya mwingine. Hakuna mwenye cheti cha kusema nchi ni yake.
Wananchi ni nyinyi hapa. Kwa hiyo nawaomba vijana wangu, msiharibu nchi yenu, msiharibu amani yenu,” amesisitiza.
Chanzo; Mwananchi